Mji mkuu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
(Elekezwa kutoka Mji Mkuu)
Rukia: urambazaji, tafuta

Mji mkuu kwa kawaida ni mji wenye makao ya serikali ya nchi fulani. Katika nchi nyingi mji huo pia ni mji mkubwa na muhimu zaidi kushinda miji mingine nchini.

Kuna nchi ambako mji mmoja umeteuliwa kuwa mji mkuu katika katiba au kwa sheria fulani. Lakini kuna nchi nyingine ambazo hakuna sheria yoyote lakini makao makuu yanaeleweka yapo mji fulani.

Nchi kadhaa zimeteua mji fulani kuwa mji mkuu kwa shabaha ya kubadilisha mwendo wa nchi au kama jaribio la kusahihisha historia yao.

Koloni za zamani kuanzisha mji mkuu mpya[hariri | hariri chanzo]

Nchi mbalimbali zilizowahi kuwa koloni zimeamua kuanzisha mji mkuu mpya kwa sababu mji mkuu wa kikoloni uliteuliwa kutokana na mahitaji ya nchi tawala ya zamani si kutokana na mahitaji ya nchi huru yenyewe. Wakati wa ukoloni mara nyingi mji kwenye pwani penye bandari uliteuliwa kuwa mji mkuu. Sababu yake ni ya kwamba kwa ajili ya maafisa wa kikoloni mawasiliano na nyumbani kwao yalikuwa muhimi sana kushinda mawasiliano na sehemu zote za nchi ya koloni yenyewe. Wakati wa ukoloni usafiri ulikuwa kwa meli, hivyo kipaumbele cha mabandari. Katika fikra za kisiasa na za kiuchumi sababu muhimu ya kuwa na koloni ilikuwa nafasi ya nchi tawala kujipatia malighafi katika koloni na kuuza bidhaa zake - yote yalitegemea mabandari. Hasara ya chaguo lile ilikuwa ya kwamba mara nyingi mabandari ni kando kabisa katika nchi zao - watu wengi wako mbali na mji mkuu.

Brazil: Hapo Wabrazil wamehamisha mji mkuu kutoka Rio de Janeiro uliyoko pwani na kandokando la eneo la Brazil kwenda mji mpya wa Brasilia kuanzia mwaka 1960. Brasilia ilijengwa mahali pasipo na mji katika miaka 1956 - 1960 BK.

Kwa nia hiyohiyo Tanzania iliamua kuhamisha mji mkuu kutoka Daressalaam uliyoko pwani la Bahari Hindi kwenda Dodoma iliyoko katikati ya Tanzania. Uhamisho huu umepangwa tangu 1967 na kutangazwa rasmi mwaka 1997 lakini haujatekelezwa bado. Ni ofisi chache za serikali zimehamia hapo. Watanzania wanaochoka na kuchelewe huku waangalie mfano wa Brazil: Katiba ya Brazil ya mwaka 1891 ilishataja mahali pa mji mkuu mpya badala ya Rio de Janeiro lakini mipango haikuanza hadi 1926 halafu ujenzi ulianza 1956!

  • Tazama chini: Nigeria, Côte d'Ivoire

Kuhamisha mji mkuu baada ya mapinduzi[hariri | hariri chanzo]

Uturuki iliamua 1923 kuhamisha mji mkuu kutoka Istanbul kwenda Ankara. Istanbul iliwahi kuwa kwa karne nyingi mji wa Masultani tena mji wa kimataifa; mapinduzi ya 1923 yalimaliza utawala wa sultani na kutangaza Uturuki kuwa jamhuri. Pia Istanbul imekuwa kandokando ya eneo la Uturuki baada ya vita kuu ya kwanza kwa sababu sehemu za magharibi zilikuwa zimepotea na kuchukuliwa na Wagiriki na Wabulgaria. Hivyo Ankara iliteuliwa iliyoko katikati ya Uturuki mpya baada ya vita.

Urusi ilihamisha mji mkuu mara mbili. Mwaka 1712 Tsar (mfalme) mrusi Peter aliamua kujenga mji mpya katika pembe la magharibi kabisa ya nchi akahamisha mji mkuu kutoka Moscow kwenda St. Peterburg mpya. Tsar Peter aliona nchi yake ilikuwa imebaki nyuma akitaja kuleta maendeleo kwa kuiga mfano wa Ulaya ya Kati na ya Magharibi. Mji mpya ya St. Peterburg ilipangwa kuwa "dirisha la Urusi la kutazama magharibi".

Baada ya mapinduzi ya 1917 Wakomunisti waliamua kufanya Moscow iwe mji mkuu kuanzia mwaka 1918. Sababu yake ni nafasi ya Moscow iliyoko ndani zaidi ya eneo la Urusi yenyewe.

Kujenga mji mkuu wa pekee katika nchi za shirikisho[hariri | hariri chanzo]

Nchi kadhaa zinazofuata muundo wa serikali ya shirikisho zimeamua kujenga mji ulioko katika wilaya au mkoa wa shirikisho ili mji mkuu usiwepo katika eneo la mkoa au dola la shirikisho fulani.

Marekani iliteua eneo la Mkoa wa Colombia kuwa mahali pa mji mpya wa shirikisho ulioitwa baadaye kwa jina la raisi wa kwanza "Washington". Mkoa wa Colombia si sehemu ya dola lolote la shirikisho la Marekani. Mji wa Washington D.C. na mkoa wa Colombia ni eneo lilelile.

Australia ilijenga mji mkuu mpya kwa sababu miji mikubwa ya Sydney na Melbourne yote yalitaka kuwa mji mkuu wa kitaifa wa Shirikisho la Australia. Mwaka 1908 eneo la Canberra lililokuwa mashambani wakati ule liliteuliwa, ujenzi wa mji mpya ulianza mwaka 1913 na serikali pamoja na bunge ilihamia Canberra mwaka 1927. Dola la shirikisho la New South Wales lilikabidhi "Eneo la Mji Mkuu wa Shirikisho" lililokuwa eneo la pekee chini ya Bunge la Australia moja kwa moja.

Nigeria iliamua mwaka 1976 kuhamisha mji mkuu wa kitaifa kutoka Lagos kwenda mahali pa katikati ya nchi. "Eneo la Mji Mkuu wa Shirikisho" limeteuliwa. Mji mpya wa Abuja ndani ya eneo hili ukawa mji mkuu wa Nigeria mwaka 1991.

Miji mikuu mbalimbali[hariri | hariri chanzo]

Afrika Kusini ina miji mikuu mitatu kikatiba: Pretoria ndipo makao makuu ya serikali, Cape Town ndipo makao makuu ya bunge, Bloemfontein ndipo makao makuu ya Mahakama Kuu.

Bolivia ina mji mkuu rasmi katika jiji la Sucre, lakini ofisi nyingi za serikali ya kitaifa zimehamia mji mkubwa wa nchi La Paz.

Côte d'Ivoire imetangaza 1983 Yamoussoukro kuwa mji mkuu wa taifa lakini hadi leo ofisi za serikali zimebaki Abijan.